John 15

 

1 "Mimi ni mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima.
2 Yeye huliondoa ndani yangu kila tawi lisilozaa matunda, na kila tawi lizaalo hulisafisha lipate kuzaa zaidi.
3 Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya ule ujumbe niliowaambieni.
4 Kaeni ndani yangu, nami nikae ndani yenu. Tawi haliwezi peke yake kuzaa matunda lisipokaa katika mzabibu hali kadhalika nanyi hamwezi kuzaa matunda msipokaa ndani yangu.
5 "Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi yake. Akaaye ndani yangu, nami ndani yake, huyo atazaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya chochote.
6 Mtu yeyote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwalo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue.
7 Mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, basi, ombeni chochote mtakacho nanyi mtapewa.
8 Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi wangu.
9 Mimi nimewapenda ninyi kama vile Baba alivyonipenda mimi. Kaeni katika pendo langu.
10 Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu, kama vile nami nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.


11 Nimewaambieni mambo haya ili furaha yangu ikae ndani yenu, na furaha yenu ikamilike.
12 Hii ndiyo amri yangu: pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda ninyi.
13 Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu atoaye uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.
14 Ninyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru.
15 Ninyi siwaiti tena watumishi, maana mtumishi hajui anachofanya bwana wake. Lakini mimi nimewaita ninyi rafiki, kwa sababu nimewajulisha yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu.
16 Ninyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba apate kuwapa ninyi chochote mumwombacho kwa jina langu.
17 Basi, amri yangu kwenu ndiyo hii: pendaneni.
18 "Kama ulimwengu ukiwachukia ninyi, kumbukeni kwamba umenichukia mimi kabla haujawachukia ninyi.
19 Kama mngalikuwa watu wa ulimwengu, ulimwengu ungaliwapenda ninyi kama watu wake. Lakini kwa vile ninyi si wa ulimwengu, ila mimi nimewachagueni kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukieni.
20 Kumbukeni niliyowaambieni: mtumishi si mkuu zaidi kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa na ninyi pia; kama wameshika neno langu, watalishika na lenu pia.
21 Lakini hayo yote watawatendeeni ninyi kwa sababu ya jina langu, kwani hawamjui yeye aliyenituma.
22 Kama nisingalikuja na kusema nao wasingalikuwa na hatia; lakini sasa hawawezi kujitetea kwamba hawana dhambi.
23 Anayenichukia mimi, anamchukia na Baba yangu pia.
24 Kama nisingalifanya kwao mambo ambayo hakuna mtu mwingine amekwisha yafanya wasingalikuwa na hatia; lakini sasa wameona niliyoyafanya wakinichukia mimi, wakamchukia na Baba yangu pia.
25 Na hivi ni lazima yatimie yale yaliyoandikwa katika Sheria yao: <Wamenichukia bure!>
26 "Atakapokuja huyo Msaidizi nitakayemtuma kwenu kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia mimi.
27 Nanyi pia mtanishuhudia kwa kuwa mmekuwa nami tangu mwanzo.

 

John 16

 

1 "Nimewaambieni hayo kusudi msiiache imani yenu.
2 Watu watawatenga ninyi na masunagogi yao. Tena, wakati unakuja ambapo kila atakayewaua ninyi atadhani anamhudumia Mungu.
3 Watawatendeeni mambo hayo kwa sababu hawamjui Baba, wala hawanijui mimi.
4 Basi, nimewaambieni mambo haya ili saa yake itakapofika mkumbuke kwamba niliwaambieni. "Sikuwaambieni mambo haya tangu mwanzo kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi.
5 Lakini sasa namwendea yule aliyenituma; na hakuna hata mmoja wenu anayeniuliza: <Unakwenda wapi?>
6 Kwa kuwa nimewaambieni mambo hayo mmejaa huzuni mioyoni mwenu.
7 Lakini, nawaambieni ukweli: afadhali kwenu mimi niende zangu, maana nisipokwenda Msaidizi hatakuja kwenu. Lakini nikienda, basi, nitamtuma kwenu.
8 Naye atakapokuja atawathibitishia walimwengu kwamba wamekosea kuhusu dhambi, uadilifu na hukumu ya Mungu.
9 Wamekosea kuhusu dhambi kwa sababu hawaniamini;
10 kuhusu uadilifu, kwa sababu naenda zangu kwa Baba, nanyi hamtaniona tena;
11 kuhusu hukumu kwa sababu mkuu wa ulimwengu huu amekwisha hukumiwa.
12 "Ninayo bado mengi ya kuwaambieni, ila kwa sasa hamwezi kuyastahimili.
13 Lakini atakapokuja huyo Roho wa kweli atawaongoza kwenye ukweli wote; maana hatasema kwa mamlaka yake mwenyewe, bali atawaambieni yote atakayosikia, na atasema mambo yatakayokuwa yanakuja.
14 Yeye atanitukuza mimi kwa kuwa atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu.
15 Vyote alivyo navyo Baba ni vyangu; ndiyo maana nimesema kwamba huyo Roho Mtakatifu atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu.


16 "Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona!"
17 Hapo baadhi ya wanafunzi wake wakaulizana, "Ana maana gani anapotwambia: <Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona?> Tena anasema: <Kwa kuwa ninakwenda kwa Baba!">
18 Basi, wakawa wanaulizana, "Ana maana gani anaposema: <Bado kitambo kidogo?> Hatuelewi anaongelea nini."
19 Yesu alijua kwamba walitaka kumwuliza, basi akawaambia, "Je, mnaulizana juu ya yale niliyosema: <Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona?>
20 Nawaambieni kweli, ninyi mtalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utafurahi: mtaona huzuni lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha.
21 Wakati mama anapojifungua huona huzuni kwa sababu saa ya maumivu imefika; lakini akisha jifungua hayakumbuki tena maumivu hayo kwa sababu ya furaha kwamba mtu amezaliwa duniani.

22 Ninyi pia mna huzuni sasa; lakini nitawajieni tena, nanyi mtajaa furaha mioyoni mwenu, na furaha hiyo hakuna mtu atakayeiondoa kwenu.
23 Siku hiyo hamtaniomba chochote. Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu, atawapeni.
24 Mpaka sasa hamjaomba chochote kwa jina langu. Ombeni nanyi mtapata ili furaha yenu ikamilike.
25 "Nimewaambieni mambo hayo kwa mafumbo. Lakini wakati utakuja ambapo sitasema tena nanyi kwa mafumbo, bali nitawaambieni waziwazi juu ya Baba.
26 Siku hiyo mtaomba kwa jina langu, na siwaambii kwamba nitamwomba Baba kwa niaba yenu;
27 maana yeye mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu ninyi mmenipenda mimi na mmeamini kwamba nimetoka kwa Mungu.
28 Mimi nilitoka kwa Baba, nikaja ulimwenguni; na sasa nauacha ulimwengu na kurudi kwa Baba."
29 Basi, wanafunzi wake wakamwambia, "Ahaa! Sasa unasema waziwazi kabisa bila kutumia mafumbo.
30 Sasa tunajua kwamba wewe unajua kila kitu, na huna haja ya kuulizwa maswali na mtu yeyote; kwa hiyo tunaamini kwamba umetoka kwa Mungu."
31 Yesu akawajibu, "Je, mnaamini sasa?
32 Wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo ninyi nyote mtatawanyika kila mtu kwake, nami nitaachwa peke yangu. Kumbe, lakini mimi siko peke yangu, maana Baba yu pamoja nami.
33 Nimewaambieni mambo haya ili mpate kuwa na amani katika kuungana nami. Ulimwenguni mtapata masumbuko; lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu!"



John 17

 

 

 

1 Yesu alipokwisha sema hayo, alitazama juu mbinguni, akasema, "Baba, saa imefika! Mtukuze Mwanao ili naye Mwana apate kukutukuza.
2 Maana ulimpa Mwanao mamlaka juu ya watu wote ili awape uzima wa milele wote hao uliompa.
3 Na uzima wa milele ndio huu: kukujua wewe uliye peke yako Mungu wa kweli, na kumjua Yesu Kristo uliyemtuma.


4 Mimi nimekutukuza hapa duniani; nimeikamilisha ile kazi uliyonipa nifanye.
5 Sasa, Baba, nitukuze mbele yako kwa ule utukufu niliokuwa nao kabla ya kuumbwa ulimwengu.
6 "Nimekufanya ujulikane kwa watu wale ulionipa kutoka duniani. Walikuwa watu wako, nawe ukanipa wawe wangu; nao wamelishika neno lako.
7 Sasa wanajua kwamba kila ulichonipa kimetoka kwako.
8 Mimi nimewapa ule ujumbe ulionipa nao wameupokea; wanajua kwamba kweli nimetoka kwako, na wanaamini kwamba wewe ulinituma.
9 "Nawaombea hao; siuombei ulimwengu, ila nawaombea hao ulionipa, maana ni wako.
10 Yote niliyo nayo ni yako, na yako ni yangu; na utukufu wangu umeonekana ndani yao.
11 Na sasa naja kwako; simo tena ulimwenguni, lakini wao wamo ulimwenguni. Baba Mtakatifu! Kwa nguvu ya jina lako ulilonipa, tafadhali uwaweke salama ili wawe kitu kimoja kama sisi tulivyo mmoja.
12 Nilipokuwa nao, mimi niliwaweka salama kwa nguvu ya jina lako ulilonipa. Mimi nimewalinda, wala hakuna hata mmoja wao aliyepotea, isipokuwa yule aliyelazimika kupotea ili Maandiko Matakatifu yapate kutimia.
13 Basi, sasa naja kwako, na nimesema mambo haya ulimwenguni, ili waweze kushiriki kikamilifu furaha yangu.
14 Mimi nimewapa neno lako, nao ulimwengu ukawachukia, kwa sababu wao si wa ulimwengu kama vile nami nisivyo wa ulimwengu.
15 Siombi uwatoe ulimwenguni, bali naomba uwakinge na yule Mwovu.
16 Wao si wa ulimwengu, kama vile nami nisivyo wa ulimwengu.
17 Waweke wakfu kwa ukweli; neno lako ni ukweli.
18 Kama vile ulivyonituma ulimwenguni, nami pia nimewatuma wao ulimwenguni;
19 na kwa ajili yao mimi mwenyewe najiweka wakfu ili nao pia wafanywe wakfu katika ukweli.
20 "Siwaombei hao tu, bali nawaombea pia wote watakaoamini kutokana na ujumbe wao.


21 Naomba ili wote wawe kitu kimoja. Baba! Naomba wawe ndani yetu kama vile wewe ulivyo ndani yangu nami ndani yako. Naomba wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba wewe ulinituma.
22 Mimi nimewapa utukufu uleule ulionipa mimi, ili wawe kitu kimoja kama nasi tulivyo mmoja;
23 mimi niwe ndani yao, nawe uwe ndani yangu; naomba wakamilishwe na kuwa kitu kimoja, ili ulimwengu upate kujua kwamba wewe ulinituma, na kwamba unawapenda wao kama unavyonipenda mimi.
24 "Baba! Nataka wao ulionipa wawe pamoja nami pale nilipo, ili wauone utukufu wangu ulionipa; kwa kuwa ulinipenda kabla ya kuumbwa ulimwengu.
25 Baba Mwema! Ulimwengu haukujui, lakini mimi nakujua. Hawa nao wanajua kwamba wewe ulinituma.
26 Nimekufanya ujulikane kwao na nitaendelea kufanya hivyo, ili upendo ulio nao kwangu uwe ndani yao, nami niwe ndani yao."

 

John 18

 

 

 

 

1 Yesu alipokwisha sema hayo, alikwenda ng'ambo ya kijito Kedroni, pamoja na wanafunzi wake. Mahali hapo palikuwa na bustani, naye Yesu akaingia humo pamoja na wanafunzi wake.
2 Yuda, aliyemsaliti Yesu, alipajua mahali hapo kwani mara nyingi Yesu alikutana na wanafunzi wake huko.
3 Basi, Yuda alichukua kikosi cha askari na walinzi kutoka kwa makuhani wakuu na Mafarisayo, akaja nao bustanini wakiwa na taa, mienge na silaha.
4 Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawauliza, "Mnamtafuta nani?"

5 Nao wakamjibu, "Yesu wa Nazareti!" Yesu akawaambia, "Mimi ndiye." Msaliti Yuda alikuwa amesimama hapo pamoja nao.
6 Basi, Yesu alipowaambia: "Mimi ndiye", wakarudi nyuma, wakaanguka chini.
7 Yesu akawauliza tena, "Mnamtafuta nani?" Wakamjibu, "Yesu wa Nazareti!"
8 Yesu akawaambia, "Nimekwisha waambieni kwamba mimi ndiye. Basi, kama mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao."
9 (Alisema hayo ili yapate kutimia yale aliyosema: "Wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja.")
10 Simoni Petro alikuwa na upanga; basi, akauchomoa, akamkata sikio la kulia mtumishi wa Kuhani Mkuu. Mtumishi huyo aliitwa Malko.
11 Basi, Yesu akamwambia Petro, "Rudisha upanga wako alani. Je, nisinywe kikombe alichonipa Baba?"
12 Kile kikosi cha askari, mkuu wake na walinzi wa Wayahudi walimkamata Yesu, wakamfunga

13 na kumpeleka kwanza kwa Anasi; Anasi alikuwa baba mkwe wa Kayafa ambaye alikuwa Kuhani Mkuu mwaka huo.
14 Huyo Kayafa ndiye aliyekuwa amewashauri Wayahudi kwamba ni afadhali mtu mmoja afe kwa ajili ya taifa.
15 Simoni Petro pamoja na mwanafunzi mwingine walimfuata Yesu. Huyo mwanafunzi mwingine alikuwa anajulikana kwa Kuhani Mkuu, hivyo aliingia pamoja na Yesu ndani ya ukumbi wa Kuhani Mkuu.
16 Lakini Petro alikuwa amesimama nje, karibu na mlango. Basi, huyo mwanafunzi mwingine aliyekuwa anajulikana kwa Kuhani Mkuu alitoka nje akasema na mjakazi, mngoja mlango, akamwingiza Petro ndani.
17 Huyo msichana mngoja mlango akamwuliza Petro, "Je, nawe pia ni mmoja wa wanafunzi wa mtu huyu?" Petro akamwambia, "Si mimi!"
18 Watumishi na walinzi walikuwa wamewasha moto kwa sababu kulikuwa na baridi, wakawa wanaota moto. Naye Petro alikuwa amesimama pamoja nao akiota moto.
19 Basi, Kuhani akamwuliza Yesu juu ya wanafunzi wake na mafundisho yake.
20 Yesu akamjibu, "Nimesema na kila mtu daima hadharani. Kila mara nimefundisha katika masunagogi na Hekaluni, mahali wakutanikiapo Wayahudi wote; na wala sijasema chochote kwa siri.
21 Kwa nini waniuliza mimi? Waulize wale waliosikia nini niliwaambia. Wao wanajua nilivyosema."
22 Alipokwisha sema hayo mlinzi mmoja aliyekuwa amesimama hapo akampiga kofi akisema, "Je, ndivyo unavyomjibu Kuhani Mkuu?"
23 Yesu akamjibu, "Kama nimesema vibaya, onyesha huo ubaya; lakini ikiwa nimesema vema, mbona wanipiga?"
24 Basi, Anasi akampeleka Yesu akiwa amefungwa, kwa Kuhani Mkuu Kayafa.


25 Petro alikuwa hapo akiota moto. Basi, wakamwuliza, "Je, nawe pia si mmoja wa wanafunzi wake?" Yeye akakana na kusema, "Si mimi!"
26 Mmoja wa watumishi wa Kuhani Mkuu, jamaa wa yule aliyekatwa sikio na Petro, akamwuliza, "Je, mimi sikukuona wewe bustanini pamoja naye?"
27 Petro akakana tena; mara jogoo akawika.
28 Basi, walimchukua Yesu kutoka kwa Kayafa, wakampeleka ikulu. Ilikuwa alfajiri, nao ili waweze kula Pasaka, hawakuingia ndani ya ikulu wasije wakatiwa najisi.
29 Kwa hiyo, Pilato aliwaendea nje, akasema, "Mna mashtaka gani juu ya mtu huyu?"


30 Wakamjibu, "Kama huyu hangalikuwa mwovu hatungalimleta kwako."
31 Pilato akawaambia, "Haya, mchukueni ninyi wenyewe, mkamhukumu kufuatana na Sheria yenu." Wayahudi wakamjibu, "Sisi hatuna mamlaka ya kumwua mtu yeyote."
32 (Ilifanyika hivyo yapate kutimia maneno aliyosema Yesu kuonyesha atakufa kifo gani.)
33 Pilato akaingia tena ndani ya ikulu, akamwita Yesu na kumwuliza: "Ati wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?"
34 Yesu akamjibu, "Je, hayo ni maneno yako au wengine wamekwambia habari zangu?"


35 Pilato akamjibu, "Je, ni Myahudi mimi? Taifa lako na makuhani wamekuleta kwangu. Umefanya nini?"
36 Yesu akamjibu, "Ufalme wangu si wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu watumishi wangu wangenipigania nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini sasa ufalme wangu si wa hapa."
37 Hapo Pilato akamwambia, "Basi, wewe ni Mfalme?" Yesu akajibu, "Wewe umesema kwamba mimi ni Mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili hiyo; na kwa ajili hiyo nimekuja ulimwenguni kuwaambia watu juu ya ukweli. Kila mtu wa ukweli hunisikiliza."
38 Pilato akamwambia, "Ukweli ni kitu gani?" Pilato alipokwisha sema hayo, aliwaendea tena Wayahudi nje, akawaambia, "Mimi sioni hatia yoyote kwake.
39 Lakini, mnayo desturi kwamba mimi niwafungulie mfungwa mmoja wakati wa Pasaka. Basi, mwataka niwafungulieni Mfalme wa Wayahudi?"
40 Hapo wakapiga kelele: "La! Si huyu ila Baraba!" Naye Baraba alikuwa mnyang'anyi.


go to chapters........1-7.......8-14.......15-18.......19-21

BOOK OF JOHN HOMEPAGE